MKUU wa Mkoa wa Manyara, Alexander Pastory Mnyeti amewataka mahakimu wa mkoa huo kutekeleza wajibu wao ipasavyo wakati wanaposikiliza kesi na kutoa hukumu kwa haki ili kuepuka malalamiko yanayotolewa na wananchi.
Akizungumza kwenye ziara yake ya kwanza ya siku saba katika Wilaya ya Simanjiro, Mnyeti alisema kupitia nafasi yake ya Mwenyekiti wa kamati ya maadili, hatakubali kuona wananchi wanalalamikia kukosa haki.
Mnyeti alisema baadhi ya mahakimu wanajigeuza kuwa miungu watu na kushindwa kutekeleza wajibu wao ipasavyo hivyo kusababisha malalamiko kwa wananchi. "Hatuwezi kukubali kuona mambo kama hayo, yakifanyika kama kuna mtu anaona kuna mahakimu siyo waadilifu wanakula rushwa na kushindwa kutoa haki nijulisheni," alisema Mnyeti.
Awali, mkazi wa mtaa wa Njiro, Theopista Paulo alisema amekuwa akinyanyasika wakati akidai haki yake. Theopista alisema mmoja kati ya mahakimu wa eneo hilo alikuwa anamwambia hata kama akimkataa na kesi yake kuhamishwa kwenye mahakama nyingine hawezi kushinda chochote.
Hata hivyo, Mwanasheria wa ofisi ya mkuu wa mkoa huo, Peter Mangala alisema mwananchi yeyote ana haki ya kumkataa hakimu endapo atakuwa na sababu za msingi. Mangala alisema endapo mwananchi akiwa na hoja za msingi anazozipinga anaweza kumkataa jaji au Hakimu atakapobaini kuwa hawezi kutendewa haki.
Wananchi wa Mji mdogo wa Orkesumet Wilayani Simanjiro Mkoani Manyara, wakitoa kero kwa Mkuu wa Mkoa huo Alexander Pastory Mnyeti.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara Alexander Pastory Mnyeti akizungumza na wananchi wa mji mdogo wa Orkesumet Wilayani Simanjiro.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...