Wakala
wa Vipimo Tanzania (WMA) chini ya usimamizi wa Wizara ya Viwanda,
Biashara na Uwekezaji imeendelea kutoa elimu kwa wakulima pamoja na
kuhakiki mizani itakayotumika kununulia zao la Pamba ikiwa ni maandalizi
ya msimu wa ununuzi wa Pamba kwa mwaka huu (2018). Zoezi hili la
utoaji elimu na uhakiki wa mizani itakayotumika kununulia Pamba
linaendelea katika Mikoa ya Shinyanga, Geita, Simiyu, Mwanza, Tabora,
Mara pamoja na Kagera kwa kushirikiana na Ofisi ya Wakala wa Vipimo
Makao Makuu.
Dhumuni kuu la utoaji elimu kwa wakulima wa zao la Pamba Kanda ya Ziwa ni kuwawezesha wakulima kutambua mizani iliyosahihi (inayoruhusiwa kwa biashara) na ile iliyochezewa (isiyoruhusiwa kwa biashara) ili waweze kujilinda wenyewe pindi maafisa vipimo wanapokuwa hawapo katika vituo vya kuuzia Pamba yao na pia ni kuwawezesha wakulima kupata faida ya thamani kamili ya jasho lao.
Dhumuni kuu la utoaji elimu kwa wakulima wa zao la Pamba Kanda ya Ziwa ni kuwawezesha wakulima kutambua mizani iliyosahihi (inayoruhusiwa kwa biashara) na ile iliyochezewa (isiyoruhusiwa kwa biashara) ili waweze kujilinda wenyewe pindi maafisa vipimo wanapokuwa hawapo katika vituo vya kuuzia Pamba yao na pia ni kuwawezesha wakulima kupata faida ya thamani kamili ya jasho lao.
Meneja
wa Wakala wa Vipimo Mkoani Mwanza, Hemed Kipengere akitoa elimu kwa
wakulima wa Pamba Wilayani Magu kuhusiana na mambo muhimu ya kuzingatia
kabla ya kupima Pamba kwenye mizani ili Wakulima waweze kupata faida ya
jasho lao la kulima Pamba.
Akizungumza na Meneja Sehemu ya Elimu, Habari na Mawasiliano Bi. Irene John, alisema katika maandalizi ya msimu mpya wa ununuzi wa Pamba Mwanza wanategemea kutoa elimu kwa Wilaya tano (5), Simiyu Wilaya tano (5), Shinyanga Wilaya tatu (3), Geita wilaya sita (6), Tabora Wilaya tatu (3) , Kagera Wilaya mbili (2) pamoja na Mara Wilaya tano (5). Hivyo, kwa mwaka huu jumla ya Wilaya 28 zimelima Pamba na zote zitapatiwa elimu inayohusu matumizi ya vipimo sahihi na faida zinazopatikana kwa mkulima kwa kuuza mazao yake kupitia mizani iliyohakikiwa na Wakala wa Vipimo.
Mwaka huu tofauti kidogo na mwaka jana maana Serikali imefufua Vyama vya Ushirika ambapo ununuzi wote wa Pamba utafanywa na Vyama vya Msingi ambayo vinasimamiwa na wakulima wenyewe badala ya kuuza Pamba yao kupitia Mawakala kama ilivyokuwa imezoeleka miaka ya nyuma. Mkulima wa Pamba atanufaika zaidi kwa kuuza mazao yake kupitia vyama vya msingi sababu mazao yote yatakayopatikana kutoka kwenye Pamba yaani mbegu pamoja na nyuzi mkulima atahusika kupata faida ya uuzaji wa mazao hayo tofauti na mwanzo faida kama hii ilikuwa haipatikani kwake isipokuwa kwa mfanyabiashara tu.
Afisa
wa Wakala wa Vipimo mkoani Mara wakionesha mizani sahihi na ile isiyo
sahihi ili wakulima waweze kujilinda wenyewe pindi maafisa wanapokuwa
hawapo.
Pia kuuza Pamba kupitia vyama vya msingi itapunguza ulaghai kwenye mizani sababu wasimamizi na watumiaji wa Mizani watakuwa ni wakulima wenyewe wa Pamba wala siyo mawakala.
Irene alisema Sheria ya Vipimo Sura 340 inawataka Wakala wa Vipimo kuhakiki na kupiga chapa vipimo vyote vinavyotumika katika biashara ikiwa ni pamoja na kuweka sticker kwa kipimo kitakachokuwa tayari kimehakikiwa na kukutwa kikiwa sahihi ili iwe rahisi kwa wakulima kuona na kutambua mizani iliyokaguliwa na kuruhusiwa kwa biashara kwa mwaka husika.
Bi. Irene ameongezea kuwa Wakala wa Vipimo itaendelea kufanya ukaguzi wa kushtukiza na wakawaida wakati wowote baada ya msimu wa ununuzi wa Pamba kuanza ili panapokuwa na malalamiko kutoka kwa wananchi kuhusu uonevu katika mizani yaweze kutatuliwa kwa haraka.
Bi. Irene John aliwasihi wakulima wanaolalamikiwa kuweka maji, kokoto pamoja na mchanga kwenye Pamba kwa ajili ya kuongeza uzito waache tabia hiyo mara moja ili kuleta biashara ya haki.
Lengo
kuu la Wakala wa Vipimo ni kumlinda mlaji ili apate faida na thamani ya
kile alichozalisha na siyo kupunjwa na wafanyabiashara
wajanjawajanja. Irene alisisitiza kuwa kwa wale watakaobainika
kuchezea mizani kwa ajili ya kuwaibia wakulima adhabu imeboreshwa
kuanzia mwaka juzi ( Nov. 2016) hivyo, faini itaanzia laki moja
badala ya elfu kumi kama ilivyokuwa imezoeleka kufikia hadi milioni
ishirini endapo mkosaji atakubali kosa. Kesi ikifikishwa mahakamani na
mlalamikiwa akakutwa kweli alikosa kulingana na ushahidi utakaokuwa
umetolewa mshitakiwa atatozwa faini kuanzia laki tatu hadi milioni
hamsini au kifungo cha miaka mitatu au vyote kwa pamoja.
Toa Maoni Yako:
0 comments so far,add yours
Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...